Je! Hawajifikirii nafsi zao? Mwenyezi Mungu hakuumba mbingu na ardhi na viliomo
ndani yake ila kwa Haki na kwa muda maalumu. Na hakika watu wengi bila ya shaka
ni wenye kukataa kuwa watakutana na Mola wao Mlezi.
Je! Hawatembei katika ardhi wakaona ulivyo kuwa mwisho wa walio kuwa kabla yao?
Nao walikuwa na nguvu zaidi kuliko wao, na wakaitimbua ardhi na wakaistawisha
zaidi kuliko walivyo istawisha wao. Na Mitume wao wakawajia na dalili zilizo
wazi. Basi hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwadhulumu, lakini walikuwa
wakijidhulumu nafsi zao.
Hukitoa kilicho hai kutokana na kilicho kufa, na hukitoa kilicho kufa kutokana
na kilicho hai. Na huihuisha ardhi baada ya kufa kwake. Na kama hivyo ndivyo
mtavyo fufuliwa.
Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili
mpate utulivu kwao. Naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika
haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanao fikiri.
Na katika Ishara zake ni kulala kwenu usiku na mchana, na kutafuta kwenu fadhila
zake. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanao sikia.
Na katika Ishara zake hukuonyesheni umeme kwa kukutieni khofu na tamaa. Na
hukuteremshieni maji kutoka mbinguni, na kwa hayo huifufua ardhi baada ya kufa
kwake. Hakika katika hayo zipo Ishara kwa watu wanao zingatia.
Na Yeye ndiye anaye anzisha uumbaji, kisha ataurudisha mara nyengine. Na jambo
hili ni jepesi zaidi kwake. Naye ndiye mwenye mfano bora katika mbingu na ardhi.
Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.
Amekupigieni mfano kutokana na nafsi zenu. Je! Katika hao iliyo wamiliki mikono
yenu ya kulia mnao washirika katika hivyo tulivyo kuruzukuni, mkawa nyinyi
katika hivyo ni sawasawa, mnawaogopa kama mnavyo ogopana wenyewe kwa wenyewe?
Namna hivi tunazipambanua Aya zetu kwa watu wenye akili.
Bali walio dhulumu wamefuata mapendo ya nafsi zao pasina kujua. Basi nani
atamwongoa ambaye Mwenyezi Mungu amemuacha apotee? Wala hao hawatakuwa na wa
kuwanusuru.
Basi uelekeze uso wako sawasawa kwenye Dini - ndilo umbile la Mwenyezi Mungu
alilo waumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo
ndiyo Dini iliyo nyooka sawa. Lakini watu wengi hawajui.
Na mnacho kitoa kwa riba ili kiongezeke katika mali ya watu, basi hakiongezeki
mbele ya Mwenyezi Mungu. Lakini mnacho kitoa kwa Zaka kwa kutaka radhi ya
Mwenyezi Mungu, basi hao ndio watao zidishiwa.
Mwenyezi Mungu ndiye aliye kuumbeni, kisha akakuruzukuni, kisha anakufisheni, na
kisha anakufufueni. Je! Yupo yeyote katika hao mnao washirikisha na Mwenyezi
Mungu afanyae lolote katika hayo? Yeye ametakasika, na ametukuka na hayo mnayo
mshirikisha naye.
Ufisadi umedhihiri bara na baharini kwa iliyo yafanya mikono ya watu, ili
Mwenyezi Mungu awaonyeshe baadhi ya waliyo yatenda. Huenda wakarejea kwa kutubu.
Na katika Ishara zake ni kuzituma pepo ziletazo bishara njema, na ili
kukuonjesheni baadhi ya rehema zake, na ili majahazi yende kwa amri yake; na
mtafute kutokana na fadhila yake, na ili mumshukuru.
Na hakika tulikwisha watuma Mitume kwa kaumu zao, na wakawajia kwa hoja zilizo
wazi. Tukawaadhibu wale walio fanya ukosefu. Na ilikuwa ni haki juu yetu
kuwanusuru Waumini.
Mwenyezi Mungu ndiye anaye zituma pepo zikayatimua mawingu, kisha akayatandaza
mbinguni kama apendavyo. Na akayafanya mapande mapande, basi ukaiona mvua
inatoka ndani yake. Anapo wafikishia awatakao katika waja wake, mara hao huwa na
furaha.
Basi ziangalie athari za rehema ya Mwenyezi Mungu, jinsi anavyo ihuisha ardhi
baada ya kufa kwake. Basi hakika huyo ndiye bila ya shaka Mwenye kuhuisha wafu.
Na Yeye ni Muweza wa kila kitu.
Mwenyezi Mungu ndiye aliye kuumbeni kutokana na udhaifu kisha akajaalia nguvu
baada ya unyonge, kisha akajaalia baada ya nguvu unyonge tena na ukongwe.
Anaumba atakavyo. Naye ndiye Mjuzi, Mwenye uweza.
Na walio pewa ilimu na Imani watasema: Hakika nyinyi mlikwisha kaa katika hukumu
ya Mwenyezi Mungu mpaka Siku ya kufufuliwa. Basi hii ndiyo Siku ya kufufuliwa!
Lakini nyinyi mlikuwa hamuijui.
Na hakika tulikwisha wapigia watu kila mfano katika hii Qur'ani. Na ukiwaletea
Ishara yoyote hapana shaka walio kufuru watasema: Nyinyi si chochote ila ni
waongo.